Friday, April 13, 2012

Hawa Hapa Hawakustaili Kuwa Sehemu ya Tume ya Katiba


 

Katiba ni ujenzi wa msingi ambao serikali na sheria hujengwa juu yake na vile vile ni utaratibu ambao wenye inchi wanatakiwa kuamua namna ya kuendesha mambo ya msingi katika nchi yao. Watanzania mtakumbuka kuwa nchi yetu  kwa sasa ipo katika mchakato wa kutengeneza katiba mpya. Mchakato wa kutengeneza katiba ni mchakato mpana na unaohitaji kushirikisha makundi yote katika jamii. Makundi haya yanaweza kushirikishwa katika nafasi na awamu mbalimbali za utengenezaji wa katiba. Mchakato wa kutengeneza katiba mpya katika nchi yetu umeanzia katika hatua ya kuwa,  kwanza na sheria ya kutengeneza katiba mpya ambayo tayari kimakosa wameibatiza kwa jina Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya Mwaka 2011. Pamoja na makosa yake sehemu ya tatu ya sheria hii inatoa mamlaka kwa Rais wa Nchi kuunda Tume ya Uundaji wa Katiba Mpya. Sehemu ya Tano inasema, Rais, baada ya kushauriana na kukubaliana na Rais wa Zanzibar, na kwa kuzingatia hali ya kijamii, kisiasa na kiuchumi iliyopo katika Jamhuri ya Muungano kwa amri itakayochapishwa katika Gazeti la Serikali, ataunda Tume.

Hivi karibuni Rais Kikwete alipokea majina toka makundi mbalimbali kwa ajili ya kufanya uteuzi wa Tume ya Katiba yenye wajumbe 32. Uteuzi huu ulipaswa kuangalia makundi mbalimbali ili kuweza kuwa sehemu ya Tume. Kimsingi ili Tume hii iweze kuja na rasimu nzuri ya katiba itakayotumika miaka mia moja ijayo na inayokidhi haja za makundi yote ya kijamii, Rais alipaswa kuzingatia sheria na kutoa kipaumbele kwa yale makundi ambayo hayana fursa nyingine kubwa ya kushiriki katika mchakato mwingine wa katiba.Mchakato wa katiba umeganyika katika awamu mbalimbali ukianzia huu wa Sheria ya Katiba, Tume na Baadaye Bunge la Katiba. Inakuwa si busara watu wale wale wakashiriki  kuongoza michako yote hiyo mitatu. Mfano wabunge wasipodhibitiwa na sheria wanaweza kuhodhi mchakato mzima na kuwafanya watu wengine waishie tu kutoa maoni.



Katika Sehemu ya 5 ya Sheria ya Kuunda Katiba mpya kabla ya kufanyiwa marekebisho mapema mwaka huu kuna baadhi ya makundi ya watu hasa viongozi wa siasa walikatazwa na sheria kuwa sehemu ya Tume. Sheria hii ilisisitiza kuwa mtu hatakuwa na sifa za kuteuliwa kuwa mjumbe wa Tume endapo mtu huyo:


a)      ni Mbunge, Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, diwani
au kiongozi wa chama cha katika ngazi zote;
b)       ni mtumishi katika vyombo vya usalama;
c)       ni mtu aliyewahi kuhukumiwa kwa kutenda kosa, au ni mtuhumiwa
katika shauri lililopo mahakamani linalohusu shitaka la kukosa  uaminifu au maadili; au
d)      si raia wa Tanzania.



Katika majadiliano yaliyofanyika bungeni juu ya  mabadiliko sheria hii miongoni mwa mambo yaliyozingatiwa ni pamoja na kutaka kuwazuia wabunge na wawakilishi wa baraza la Zanzibar kuwa wajumbe wa bodi.  Mhe Angellah J. Kairuki makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria  Bungeni  alikunukuliwa Bungeni akisema, Serikali ilikubali kufanya marekebisho zaidi kwenye kifungu hicho ili kizuizi kiwe kwa Mbunge na Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar kama inavykuwainaonekana kwenye jedwali la Marekebisho ya Sheria hii. Kabla ya kutoka kwa sheria iliyofanyiwa mabadiliko na kwa mujibu wa majadiliano ya bunge  ilikuwa  ni wazi kuwa wabunge na wawakilishi walizuiwa   kuwa wajumbe wa tume.Mhe Kairuki alisem;

“Mheshimiwa Spika, Kamati inakubaliana na mapendekezo ya Serikali ya kuondoa maneno “au Kiongozi wa Chama cha Siasa wa ngazi zote” kutoka katika Kifungu cha 6(5)(a) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba (Namba 8) ya Mwaka 2011. Kamati ilielezwa na Serikali kwamba, mabadiliko haya yanalenga kuondoa kizuizi kwa baadhi ya watu ambao siyo Wabunge au Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar au Madiwani kutoteuliwa kuwa Wajumbe wa Tume. Hata hivyo, baada ya majadiliano, Serikali ilikubali kufanya marekebisho zaidi kwenye kifungu hicho ili kizuizi kiwe kwa Mbunge na Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar kama inavyoonekana kwenye jedwali la Marekebisho”.



Kinachosikitisha ni kwamba  wabunge pengine kwa kuwa na hamu ya kutaka wawepo kwenye kamati  ya katiba , walipingana na mapendekezo ya kamati ya kutaka wabunge  na wawakilishi wasiwe sehemu ya tume. Sheria ya katiba mpya iliyofanyiwa marekekebisho bungeni ilisainiwa na Rais  na kile kipengele cha kuwazuia wabunge na wawakilishi wasiwe wajumbe wa tume kikafutwa kwa ridhaa ya wabunge katika Mkutano wa sita tarehe 9 Februari 2012. Kwa sasa kifungu cha 6 (5) cha sheria hiyo kinamtaka Rais  Katika kufanya uteuzi wa wajumbe wa Tume kwa kutowateua watu wafuatao;



(a)    mtumishi katika vyombo vya usalama;

(b)   mtu aliyewahi kuhukumiwa kwa kutenda kosa, au ni mtuhumiwa katika shauri lililopo mahakamani linalohusu shitaka la kukosa uaminifu au maadili; au

(c)    si raia wa Tanzania.



Ni dhahiri kuwa bunge letu halina nguvu ya kutunga sheria wanazotaka  wanachi bali pengine sheria zingine hutungwa kwa maslahi binafsi  au ya vyama. Hakukuwa na sababu ya msingi kwa wabunge kujipigia debe kwa wao kuwa sehemu ya tume ilhali wanafahamu wanamajukumu mengi ya kibunge.Tume ya katiba itatumia muda mwingi kukuksanya maoni  na baadaye kuandika rasimu.  Sasa iweje leo wabunge msimame bungeni na kubadilisha sheria ili Rais awateue baadhi yenu kwenye tume. Tunawashauri wabunge wakati mwingine tuache maslahi binafsi au uchama tunapojadili mambo ya msingi kama haya.

Hivi karibu Rais Kikwete alitangaza wajumbe 30 wa Tume hii pamoja na Mwenyekiti wa Tume ambaye ni Jaji Sinde Warioba na Makamu Mwenyekiti Jaji Mkuu Mstaafu Agustino Ramadhani.Wajumbe  wa tume toka Tanzania Bara wanaowawakilisha zaidi ya watu milion 40 na Mikoa si chini ya 20  ni  wajumbe15 tu.Wajumbe hawa ni Prof. Mwesiga L. Baregu, Nd. Riziki Shahari Mngwali, Dr. Edmund Adrian Sengodo Mvungi, Nd. Richard Shadrack Lyimo, Nd. John J. Nkolo, Alhaj Said El- Maamry, Nd. Jesca Sydney Mkuchu, Prof. Palamagamba J. Kabudi, Nd. Humphrey Polepole, Nd. Yahya Msulwa, Nd. Esther P. Mkwizu, Nd. Maria Malingumu Kashonda, Mhe. Al-Shaymaa J. Kwegyir (Mb), Nd. Mwantumu Jasmine Malale Na Nd. Joseph Butiku.

 Wajumbe wengine wanaowakilisha sehemu nyingine ya nchi yenye wanachi wasiofika milion moja (Tanzania Visiwani) nao pia ni wajumbe 15. Wajumbe hao ni Dkt. Salim Ahmed Salim, Nd. Fatma Said Ali, Nd. Omar Sheha Mussa, Mhe. Raya Suleiman Hamad, Nd. Awadh Ali Said, Nd. Ussi Khamis Haji, Nd. Salma Maoulidi, Nd. Nassor Khamis Mohammed, Nd. Simai Mohamed Said, Nd. Muhammed Yussuf Mshamba, Nd. Kibibi Mwinyi Hassan, Nd. Suleiman Omar Ali, Nd. Salama Kombo Ahmed, Nd. Abubakar Mohammed Ali na  Nd. Ally Abdullah Ally Saleh. Kitendo cha kufanya uteuzi kwa kutokuwaangalia mtawanyiko wa wananchi kijiografia nao umechangia kuwepo kwa watu wengi (nusu ya wajumbe) toka eneo dogo la nchi na wanaowawakilisha wanachi wachache.

 Uteuzi huu unakinzanzana na vitu ambavyosheria ilimtaka Rais kuzingatia pale anapoteua wajumbe wa tume. Mathalan sheria inamtaka Rais Kwa kuzingatia masharti ya kifungu kidogo cha (3) cha sheria hii ya uundaji wa katiba mpya, muundo wa Tume utazingatia msingi wa kuwepo kwa uwakilishi ulio sawa kwa kila upande wa Jamhuri ya Muungano. Kosa lililofanyika ni kutafsiri neno “Uwakilishi Uliosawa” bila kuzingatia sharti la kijiografia na mtawanyiko wa watu kama jinsi sheria inavyosema.Hapa Uwakilishi uliosawa umechukuliwa kama vile ni lazima wajumbe nusu watoke Tanzania Visiwani na wengine nusu Tanzania Bara.

Katika kufanya uteuzi wa wajumbe wa Tume, Rais alipaswa kuzingatia masuala yafuatayo: uzoefu katika kufanya mapitio ya katiba na sifa za kitaaluma za wajumbe kwenye mambo ya katiba, sheria, utawala, uchumi, fedha na sayansi ya jamii;  pili jiografia na mtawanyiko wa watu katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na  pia umri , jinsia na uwakilishi wa makundi ya kijamii.

Kwa muundo wa tume suala la uwakilishi  haukupewa kipaumbele zaidi. Makundi kama ya wanawake hayana uwakilishi wa kutosha, makundi ya jamii za pembezoni na kundi la vijana navyo pia havijapata uwakikilshi katika Tume.Vijana ambao ndio wanamuda mrefu wa kuitumikia katiba hiyo mpya hawana uwakilishi wa kutosha kwenye tume hii.Pamoja na kwamba kuna kigezo cha uzoefu katika suala la sheria na katiba, bado haitoshi kuwa sababu ya kutozingatia kudi la vijana katika tume ya katiba.

Tofauti  na Mapendekezo ya Kamati ya Bunge ya Sheria na Katiba,  lakini kwa ridhaa ya wabunge kupitia Sheria ya katiba mpya iliyofanyiwa mabadiliko Februari 2012 Rais amewateua baadhi ya wajumbe ambao ni wabunge na wawakilishi. Wajumbe hawa ni Mhe. Al-Shaymaa J. Kwegyir (Mb) Tanzania Bara na Raya Suleiman Hamada mwakilishi Baraza la Wawakilishi Zanzibar. Kiuhalisia watu hawa hawakupaswa kuwa wajumbe wa tume ya katiba kwa sababu mbalimbali zikiwemo za kuwa tayari wanafasi kushiriki mchakato huu kwa kofia nyingine kama kushiriki Bunge la katiba na pia wanamajukumu ya kiuwakilishi hivyo watashindwa kufanya majukumu yao vizuri kipindi cha kukusanya maoni.

 Hivyo kwa uchambuzi huu tume hii ya katiba mpya kimsingi ina watu ambao hawakupaswa kuwa wajumbe kutokana na sababu mbalimbali zilizoelezwa hapo juu.Wengine pia wameshatambulika na jamii kama watu wasiopenda kuona mabadiliko ya kikatiba kwa maslahi ya umma kama ilivyojitokeza katika kesi mbalimbali ikiwemo ya mgombea binafsi. Ni vyema kabla ya kuanza kutenda kazi yake tume hii ikatazamwa upya.

Onesmo Olengurumwa-Mjukuu wa Nyerere, Mjomba wa Madiba,Mwanafunzi wa Luther King, Mfuasi wa Lenin na Mtoto wa Sokoine. olengurumwa2@yahoo.co.uk